Zungumza Ili Upone

Susan Njana - Wisdom&Wellness Counselor (TEWWY)

Masimulizi

by Susan Njana (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).

Katika maisha tunatakiwa tusione aibu kuyasema matatizo yetu yanayotusumbua. Tunatakiwa tutue mizigo hasi (toxic) tuliyoibeba moyoni. Kwa kawaida, binadamu ni msiri na wengine huwa ni waoga kuzungumzia au kuweka bayana matatizo yao wanayoyapata.

Haijalishi tatizo hilo ni kubwa ama dogo kiasi gani. Inategemea moyo wako umelibebabje ama una uwezo kiasi gani wa kulibeba hilo tatizo. Kama ni tatizo linalokusumbua, hata kama ni la aibu kiasi gani, ni vema ukachagua mtu wa kumshirikisha ili aweze kukusaidia kulitatua ama kukupatia ushauri.

Binadamu siyo kisiwa, tunaishi na watu. Hatuwezi kukosa mtu, angalau hata mmoja kwenye jamii tunayoishi wa kumshirikisha yetu ya moyoni kwa ajili ya kupata ushauri. Kukaa na mizigo moyoni huweza kusababisha matatizo makubwa huko mbeleni, ikiwa ni pamoja na msongo wa mawazo ambao mwisho wake unaweza ukakufikisha pabaya, na hata kufikia hatua ya kujiondoa uhai.

Tupo hapa duniani ili tusaidiane vile tunavyoweza. Katika hali ya kawaida, tunapaswa kutambua na kuguswa na matatizo ya wenzetu ili pale wanapopata tuweze kutoa msaada. Wengi hukaa na matatizo yao moyoni kwa kukosa mahali pa kuyatulia.

Hali kadhalika, napenda kusisitiza kuwa tusiruhusu mioyo yetu kubeba mizigo mizito ambayo mwisho wake huwa ni hatari. Pakua mizigo uliyokuwa nayo kwa kumwambia mtu unayemuamini ili akusaidie. Hata ikibidi, piga kelele kama njia ya kuondoa mizigo hiyo. Nikiongelea kupiga kelele, kunanikumbusha watoto wa Princes Diana wa Uingereza walipoanzisha kampeni ya “Shout”, ikiwa na maana “piga kelele” pale mizigo inapokuwia mizito moyoni mwako. Cha msingi, “usikae kimya” kwani kwa kufanya hivyo utakuwa unajiumiza sana na mwishowe itakuwa hatari kwa maisha yako.

Haijalishi wewe ni wa jinsia gani, uwe mwanaume au mwanamke, sisi sote ni binadamu, maumivu ni yale yale kwa jinsia zote. Mila na desturi nyingi zinawataka wanaume wasilie ama kupayuka hata kama wamefiwa. Mila hii ni mbaya mno. Ndio maana vifo vitokanavyo na watu kujiua ni vingi sana kwa wanaume ikilinganishwa na wanawake. Na tuivunje mila hiyo, ni potofu. Mwanaume ana haki ya kulia sawa sawa na mwanamke. Mwanaume hana moyo ama hisia tofauti na za mwanamke. Wewe mwanaume, usihifadhi mambo mazito moyoni mwako. Zungumza, omba ushauri, usijianzishie ugonjwa wa sonoma bure. Hakuna kisichoweza kupata usaidizi ama ufumbuzi chini ya jua. Epuka mateso makubwa na ya muda mrefu au kifo kutokana na kuficha ficha machungu yako.

Hivyo, katika maisha, kwa tatizo lolote liwalo, ni vizuri kushirikisha watu sahihi ili uweze kupata suluhisho mapema na kuepusha madhara au hasara inayoweza kujitokeza. Mwaka 2023 uwe ni mwaka wa kufunguka na kutua mizigo mizito itusumbuayo mioyoni mwetu. Tujitahidi kuondoa msongo wa mawazo kwa kuzungumza na wale tunaowaamini.

Maisha bila msongo wa mawazo inawezekana endapo tutazungumza na kupata msaada kutoka kwa washauri.

The Healing Hands Project

The Healing Hands empowers people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community – alleviating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain free mental health services in underserved communities and promote the economic empowerment of trained grandmothers who implementing #WHO #mhGAP evidence-based psychosocial interventions. The project provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources, referrals, advocacy and awareness raising delivered through arts. Clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection

Previous
Previous

Aisifuye Mvua, Imemnyea

Next
Next

Akipenda Chongo Huita Kengeza