Hasira Haina Nidhamu

Simulizi
by Alfreda George (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Sababu mojawapo ya mifarakano mingi inayotokea kwenye jamii nyingi inatokana na hasira. Hasira haina nidhamu. Hasira huwa haina mpangilio wowote. Mara nyingi, hasira hutokea kwa sababu ya uchonganishi ambao unatoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine.
Kulikuwa na dada mmoja ambaye alikuwa ameolewa na mwanaume ambaye Mungu alikuwa amemjalia uwezo wa kipato. Yule dada alikuwa na rafiki yake ambaye, waswahili wanasema ni rafiki wa kupika na kupakua. Habari zake nyingi alikuwa akimwambia huyo rafiki yake. Kutokana na uwezo aliokuwa nao mumewe, kumbe yule rafiki yake alikuwa hapendezwi. Alikuwa anamuonea wivu. Matokeo yake, alipanga njama ya kumharibia mambo kwa mume wake. Kwa husuda, alimwambia rafiki yake kuwa mume wake ana kimada. Hivyo inabidi amshughulikie kisawasawa. Ukweli ni kwamba hayo aliyomwambia rafiki yake yalikuwa hayana ukweli. Yote aliyonena, yalikuwa ni uongo mtupu.
Baada ya kusikia hayo, yule dada alimuomba ushauri wa nini afanye. Kwa furaha aliyokuwa nayo moyoni, rafiki yake huyo alimshauri shoga yake kuwa ni vema naye akawa na mtu wake wa pembeni ili naye amkomoe mume wake. Aliendelea kwa kusema kuwa yuko tayari kumtafutia mtu ili awe naye. Alimfariji na kumwambia asipate tabu wala nini, atamsaidia pasina shaka.
Kwa hasira alizokuwa nazo yule dada, alikubaliana naye. Hakujali yanayoweza kumtokea huko mbeleni. Wakati akitekeleza ushauri aliopewa na rafiki yake, nidhamu ndani ya nyumba ikaanza kupungua. Mume akimuuliza kitu, anakuja juu vibaya hadi mume akaanza kugundua na kuhisi kuwa kinachoendelea si sawa, ipo namna.
Mbaya zaidi rafiki yake yule yule alimueleza mume wa rafiki yake kila kitu, yaani mambo yale ya bwana wa pembeni. Hatimaye, maisha ya huyo dada yalianza kuwa magumu kupita kiasi. Pamoja na kwamba mume hakumwacha, maisha yake yaligeuka na kuwa magumu kupindukia. Yalikuwa machungu kama shubiri. Cha kushangaza, alipomlalamikia rafiki yake kuhusu mabadiliko ya maisha mle ndani kwake, majibu yake hayakuwa na mwelekeo wa masikitiko. Alimwambia kuwa avumilie tu kwani maisha ndivyo yalivyo, hupanda na kushuka. Aliendelea kwa kusema kuwa watu wakiwa pamoja hawakosi kupishana mara moja moja. Aliongeza kwa kusema hata vyombo kabatini navyo huwa vinagongana, sembuse binadamu!
Tabia hii inashangaza sana na inatoa picha Kamil I ya binadamu jinsi walivyo. Matatizo yote anayopata dada huyu ni kutokana na roho mbaya ya yule rafiki yake. Chanzo cha yote haya ni yule rafiki yake ambaye amekuwa akiuma huku na kule, kwa lengo la kuchonganisha ili wanandoa hao waachane.
Yatupasa tuwe makini tunapopewa ushauri na binadamu wenzetu. Endapo huyu dada angeyafanyia kazi maneno ya rafiki yake na kuyachambua kwa kina asingefikia hapo alipo sasa. Masikini dada wa watu, amebaki katika hali ya majonzi, kutahayari na kuchanganyikiwa hata asijue la kufanya.
Katika maisha inakubidi uangalie akili yako inabeba nini, na wakati gani. Maamuzi yako ni budi yatawaliwe na moyo wako. Kumbuka, siyo kila rafiki ni rafiki wa kweli, ama rafiki mwaminifu kwako. Marafiki wengine huwa hawawatakii wenzao mambo mazuri. Jihadhari sana, kuwa makini na uwe mbali nao pale unapoona dalili za kuchonganisha zinaanza kujitokeza.
The Healing Hands Project
The Healing Hands empowers people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community – alleviating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain free mental health services in underserved communities and promote the economic empowerment of trained grandmothers who implementing #WHO #mhGAP evidence-based psychosocial interventions. The project provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources, referrals, advocacy and awareness raising delivered through arts. Clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection