Umakini Katika Kufanya Maamuzi ni Muhimu

Masimulizi ...
by Margaret Kayombo (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Hapo zamani za kale, baada ya kuumbwa ulimwengu na vitu vyote ndani yake pamoja na watu. Mungu alifikiria sana juu ya uhai wa wanadamu. Alifikiri endapo itakuwa sahihi iwapo wanadamu wataishi milele bila kufa kama yeye Muumba au wafe baada ya kuishi ulimwenguni kwa muda fulani. Baada ya fikra hizo, hatimaye aliwatuma viumbe wawili wakawaambie wanadamu kuwa yawapasa wafanye maamuzi wenyewe kuhusu fikra zake hizo.
Kwanza alimtuma kinyonga na kumpa ujumbe huu. Kinyonga aliupokea ujumbe na kuelekea ardhini. Aliwaambia binadamu kama alivyoagizwa na Mungu kwa kusema: “Mmeambiwa msizaane, mbaki nyie wawili tu ulimwenguni, mke na mume na msife ila muishi milele”
Kisha Mungu akamtuma njiwa na ujumbe ambao ulikuwa tofauti na ule aliopewa kinyonga. Njiwa alianza kwa kuwaambia wanadamu: “Mungu ameniagiza niwaambie kuwa mkitaka mzaane kisha mfe. Mkifa uhai utaendelezwa na watoto, wajukuu, vitukuu, vilembwe, vilembekeza na vinying’inya vyenu”. Njiwa aliendelea kusema, “Kwa jinsi hiyo, ijapokuwa nyinyi wenyewe mtakufa, dunia haitakuwa tupu bali itaendelezwa na hao mtakaowazaa na watakaowazaa na watakaozaliwa. Nanyi mtakumbukwa milele.”
Pamoja na kwamba kinyonga alikuwa wa kwanza kutumwa na Mungu, kwasababu ya mwendo wake wa pole pole, mbele na nyuma, alifika muda moja na Njiwa. Kinyonga alipofika alianza kutoa ujumbe wake na watu walimkemea na kumcheka kwa kuwacheleweshea ujumbe wao. Hawakuwa na subira hivyo hawakumtaka kinyonga azungumze. Walimruhusu njiwa atoe ujumbe uliotoka kwa Mungu kabla ya Kinyonga hajafanikiwa kufanya hivyo. Chapuchapu Njiwa alitoa ujumbe wake kama alivyoagizwa. Alifanikisha kuuwasilisha japo ulikuwa mrefu lakini ujumbe uliwafikia. Wakausikiliza kwa makini, wakauona ni ujumbe mzuri, wakaukubali. Walipokubali tu, Kinyonga naye akakubaliwa kuuhitimisha ujumbe wake aliokuwa ameanza kuutoa na akasitishwa asiendelee. Baada ya binadamu kuusikiliza ujumbe wa kinyonga waliuona kuwa ni mzuri kuliko ule wa njiwa kwani kama wangeuchagua wasingekuwa wanakufa, wangeishi milele. Walitaka kuubadilisha uamuzi wao kwani ni dhahiri kuwa watu hawapendi kufa.
Hapo sauti ya Mungu ikasikika ikisema kwamba kubadilisha haiwezekani, sababu alikuwa amekwishapokea tayari uamuzi wao na tayari ameukubalia. Binadamu walipotaka kumuuliza maswali maswali sauti hiyo ilitoweka ghafla hivyo hawakuweza kufanya chochote. Muda ulikuwa umekwisha. Hivyo basi kuanzia hapo wanadamu wakaanza kuzaana na kufa.
Kuna mengi ya kujifunza hapa.
- Tuwe waaminifu na kutimiza wajibu wetu kwa wakati.
- Tufikirie kwa makini kabla ya kufanya maamuzi
- Tusiwe vigeugeu wakati wa kutoa maamuzi yaliyo sahihi.
- Tuishi na kujua daima kwamba yupo mwenye maamuzi ya mwisho juu ya kila kitu.
The Healing Hands Project
The Healing Hands project will economically empower people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community - eliminating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain the implementation of accessible psychosocial interventions in underserved communities and promote the economic empowerment of the grandmothers who have been trained in and are implementing WHO's mental health Gap Action Program. Healing Hands provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources delivered through arts, where clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection to stay up-to-date.
#MentalHealth #Grandmother #Wisdom #Wellness #mhGAP #HealingHands #Art #Culture #Tanzania