Pole Pole Ndio Mwendo

Simulizi
by Alfreda George (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Maisha ya mwanadamu yanatakiwa yawe na mpangilio. Hakuna njia ya mkato katika maisha. Yatupasa kujifunza kutoka kwa shuhuda mbalimbali, shuhuda zinazoelezea mapito ya watu mbali mbali, shuhuda zinazoweza kukujenga, hata na wengine pia.
Maisha ni kuanzia chini kwenda juu. Hata nyumba huanzia kwenye msingi. Maisha kwa watu walio wengi, hususan vijana yanakosa msingi. Kwa mfano, vijana wengi huwa wanataka wakianza kazi, mara moja wawe na gari, nyumba na maisha mazuri.
Kwa upande wa mabinti, hali ni hivyo hivyo. Wengi hutaka maisha mazuri kuliko uwezo wao. Mathalan, kama wakitaka kuolewa wangependa kuolewa na watu ambao ni matajiri, wenye magari, nyumba na vitu vingine vingi vya thamani na anasa. Kwa kawaida mabinti hawa huwa hawachunguzi na wala kujali kabisa namna utajiri huo ulivyopatikana. Cha msingi, wao wanachotaka ni kuishi maisha ya anasa kwa njia yoyote iwayo.
Mara nyingi mali usiyoihangaikia huwa haina uchungu. Binti akipata fursa ya kuolewa na mtu tajiri anaweza akafuja mali alizozikuta. Kwa uhakika hatakuwa na uchungu navyo.
Inashauriwa kuwa kila mtu inampasa akubali kuanza maisha na sifuri kwani huo ndio ukweli wenyewe. Hakuna mtu yeyote anayezaliwa na chochote. Jitihada za mtu binafsi ndizo ziwezazo kumuinua hadi akafika ngazi fulani.
Kuwa na mawazo ya kutaka kutajirika haraka haraka bila jitihada zozote ni kujidanganya. Mara nyingi tunaona vijana waliopata utajiri kwa njia za mkato wakishindwa kuthamini utajiri wao. Hali kadhalika, tunaona maisha ya vijana wengi yanatawaliwa na majivuno na jeuri maana hawana uchungu na vitu walivyovipata kupitia njia ya mkato ama za udanganyifu.
Nawaasa vijana kuwa wajifunze kutoka kwa shuhuda zinazotolewa na wahenga. Maisha ni mchakato, hayana njia ya mkato. Napenda kuwapa ushuhuda wangu mwenyewe. Nilianza kazi nikiwa sina chochote, hii haikuwa ajabu kwangu kwani kwa wengi huwa ni hivyo. Nililala chini wiki mbili ndipo nikapata tandiko na kitanda. Maisha hayo nayakumbuka hadi leo. Usisononeke unapokutana na maisha magumu mwanzoni, sote hupitia huko. Chukua jitihada za kufanya kazi kwa bidii. Pengine itakuchukua muda mrefu kupata mafanikio. Usikate tamaa kwani “Polepole Ndio Mwendo”, ipo siku utafika tu. Wahenga pia walisema “Haraka Haraka Haina Baraka.”
Kijana, tulizana. Binti tulizana. Maisha ya kurukaruka hayana baraka. Tafuteni kwa njia za halali na siyo njia za mkato.
The Healing Hands Project
The Healing Hands project will economically empower people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community - eliminating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain the implementation of accessible psychosocial interventions in underserved communities and promote the economic empowerment of the grandmothers who have been trained in and are implementing WHO's mental health Gap Action Program. Healing Hands provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources delivered through arts, where clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection to stay up-to-date.
#MentalHealth #Grandmother #Wisdom #Wellness #mhGAP #HealingHands #Art #Culture #Tanzania