Wazazi Wapendeni Watoto Wenu Sawa

Victoria Nakajumo - Wisdom&Wellness Counselor (TEWWY)

Simulizi ...

by Victoria Nakajumo (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).

Kuna familia ilibahatika kupata watoto 4, kati yao 2 wakiume na 2 wakike. Uzazi wao wa pili walipata watoto mapacha, wakike na wakiume. Ilitokea kwamba mama alitokea kumpenda sana pacha wa kike, mpaka akawa anamshirikisha siri zake zote. Binti naye alifanya vivyo hivyo, alimshirikisha mama yake kila kitu.

Pacha wa kiume alikuwa hampendi, kiasi kwamba huyu mama hata anapokaa na wamama wenzake alikuwa hamuongelei kwa uzuri. Walipohitimu kidato cha nne, pacha wa kiume hakufanya vizuri kama yule wa kike. Kufeli kwake kulimzidishia chuki mama yake dhidi ya huyo pacha wa kiume. Bila aibu, mama huyu alizidisha na kuendeleza tabia ya kutokumpenda na kumsemasema vibaya kwa watu.

Kwa bahati nzuri, binti alipata kibarua kwenye duka la mtu tajiri ambaye alikuwa na familia yake, yaani mke na watoto. Siku zilivyozidi kwenda, binti alijikuta anaingia kwenye mahusiano ya kimapenzi na tajiri yake. Tajiri naye alizama kwenye wimbi la mapenzi na binti huyu. Akaanza kumpa pesa za kukarabati nyumba ya wazazi wake. Katika hali ya kawaida huyu mama angeshituka binti kupewa fedha nyingi kiasi kile na tajiri yake. Angejiuliza sababu za binti yake kukirimiwa hivyo na mtu baki. Badala yake alizidi kumpenda sana binti yake. Pamoja na kwamba mama alikuwa anajua kila kitu kuhusu yale aliyokuwa anatenda binti yake hususan kuvuruga ndoa ya watu, bado alizidi kumpenda. Kwa maana hiyo alibariki mahusiano haya haramu kwa sababu ya misaada waliyokuwa wanaipata.

Kwa bahati mbaya binti alikutwa na umauti, alifariki. Kifo cha binti huyu kilimuumiza sana mama. Mwanaye kipenzi ndio alikuwa kila kitu kwake, na ndiye aliyekuwa anakaa naye hapo nyumbani. Yule pacha wakiume na wale watoto wengine walikuwa wanafanya kazi mikoani.

Baada ya kumaliza msiba, watoto walirudi makwao. Mama yao kwa upweke aliokuwa nao, aliomba angalau mtoto mmojawapo arudi Dar ili akae naye. Lakini kwa bahati mbaya ilishindikana, haikuwezekana. Badala ya kuichunguza nafsi yake na kujiuliza kulikoni iwe ngumu kwa mtoto angalau mmoja kuwa tayari kukaa naye, alianza kulalama na kuuliza kwa nini wanamuacha wakati yeye ni mama yao. Aliwaambia maneno mengi ya kuwalaani watoto hawa, Lakini ukweli ni kwamba “Dua la Kuku Halimpati Mwewe.”Mama aliachwa peke yake na wanaye wasiopendwa walimuacha aendelee na malalamiko yake.

Tunajifunza nini kutoka mazungumzo haya?

  1. Wazazi tuwapende watoto wetu wote sawasawa.
  2. Kwa mzazi, watoto wote ni sawa, tusiwabague.
  3. Tumeona adhabu ya kubagua watoto ilivyompata mama huyu. Alibakia na upweke, na pengine alikufa akiwa peke yake.

Tujifunze kutoka kwa huyu mama, yasije yakatukuta ya hivyo. Mara nyingi kwenye misiba tumesikia wafiwa wanapolia, hususan akina mama wanasema, “kwa nini Mungu umemchukua mwanangu huyu, si bora hata ungemchukua huyo mwingine”!! Maneno kama haya huwaumiza sana wale wanaobakia nyuma, hujiona hawana thamani na hivyo hujenga ukuta mkubwa sana baina yao na mama yao mzazi.

The Healing Hands Project

The Healing Hands project will economically empower people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community - eliminating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain the implementation of accessible psychosocial interventions in underserved communities and promote the economic empowerment of the grandmothers who have been trained in and are implementing WHO's mental health Gap Action Program. Healing Hands provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources delivered through arts, where clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection to stay up-to-date.

#MentalHealth #Grandmother #Wisdom #Wellness #mhGAP #HealingHands #Art #Culture #Tanzania

Previous
Previous

Mkono Mtupu Haulambwi

Next
Next

Tusiwadharau Watoto, Wanaweza Kuwa Walimu Wetu Pia