Tuache Kulea Watoto Kama Mayai

Simulizi
by Caroline Swai (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Hapa duniani kila mtu anapita kwa wakati wake. Katika maisha ya kawaida, tunatamani watoto wetu wapate mahitaji muhimu ikiwa ni pamoja na chakula, elimu nzuri, kazi nzuri na hatimaye kuoa/kuolewa na kuwa na familia. Lakini sisi kama wazazi kuna wakati tunafanya makosa kwa kujifanya tunawapenda sana watoto wetu hadi kupitiliza. Kwa kufanya hivyo, kumbe tunawaharibia maisha yao ya baadaye.
Simulizi hii ni ya kweli, inamhusu mama mmoja ambaye alimpenda sana mwanae wa kike hadi kupitiliza. Mama huyo alimdekeza vibaya mtoto huyo kiasi kwamba alikuwa anafanyiwa kila kitu na dada wa kazi. Kwa vile alikuwa anafanyiwa kila kitu, binti huyo hakujua mambo mengi muhimu na ya msingi, kama vile kufagia ndani, kupiga deki, kuoga mwenyewe, kufua nguo zake na hata zile za ndani, kupika na kadhalika.
Kwa bahati nzuri msichana alisoma vizuri hadi chuo ila shida ni kuwa alikuwa mvivu hawezi kufanya chochote. Hali hiyo ilifanya chumba chake kinuke kutokana na kutofagiliwa, kutotandika kitanda, nguo kuwa chafu na kila kitu chumbani kwake kukosa mpangilio maalum. Msichana alifanikiwa kumaliza chuo na kwa kuwa Mungu si Athumani, alipata mchumba na ilifanyika harusi ya kifahari ambayo kila mtu aliisifia.
Kasheshe ilianza baada ya fungate. Bi harusi hakujua aanzie wapi. Kutokana na mapenzi kuwa bado mapya, mume alijitahidi kumsaidia na kumfichia siri mkewe. Lakini kutokana na binti kutojua kila kitu ambacho anatakiwa kutekeleza kama mke, mume huyu uzalendo ulimshinda. Ilimlazimu kufanya maamuzi magumu, alimrudisha mke wake kwao ili akafundishwe kazi zote zinazomhusu, hususan, zile za ndani. Mume aliahidi kuwa akishazijua kazi hizo, atakuja kumchukua kwani alikuwa bado anampenda sana.
Ilikuwa ni aibu tupu kwa mama yake na binti. Ilimlazimu mama afanye kazi ya ziada ya kutafuta watu wa kumweka sawa binti yake kwa kuwalipa. Baada ya miezi mitatu binti alifuzu na kukidhi vigezo vya kuwa mke bora. Mume alienda kumchukua na sasa wanaishi kwa furaha na amani. Kuna mengi ya kujifunza kutokana na hadithi hii. Wazazi, hususan akina mama, tunatakiwa kuwa makini katika malezi ya watoto wetu. Kama ule usemi wa “tumkunje samaki angali mbichi" ndivyo inavyotakiwa tufanye, vinginevyo itakuwa vigumu kumkunja akishakauka. Samaki akikauka, ukimkunja atavunjika vunjika vibaya.
Pia tusiwalee watoto kama mayai tukiogopa yatavunjika. Tuwafundishe kazi zote muhimu za nyumbani ili kuondoa usumbufu wa baadaye, kuweka heshima ya binti zetu kwa waume zao na kuokoa gharama zitakazojitokeza baadaye endapo atakuwa hajui kazi yoyote tangu mwanzo. Yatupasa watoto wote, wasichana na wavulana wafundishwe kazi zote muhimu kwani hatutaishi nao milele. Hii ni kwa kwa faida yao wenyewe. Pia simulizi hi inaendana na methali inayosema "usipoziba ufa utajenga ukuta".
The Healing Hands Project
The Healing Hands project will economically empower people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community - eliminating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain the implementation of accessible psychosocial interventions in underserved communities and promote the economic empowerment of the grandmothers who have been trained in and are implementing WHO's mental health Gap Action Program. Healing Hands provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources delivered through arts, where clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection to stay up-to-date.
#MentalHealth #Grandmother #Wisdom #Wellness #mhGAP #HealingHands #Art #Culture #Tanzania