Chiriku Na Panzi

Simulizi
by Margaret Kayombo (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Panzi ni mdudu anayependwa na watoto wengi. Watoto humkimbiza na wakimshika. hupenda kumchezea. Panzi anapenda kuishi kwenye nyasi.
Siku moja, Panzi alikuwa akirukaruka kwenye shamba la mpunga. Mara alitokea ndege kwa lengo la kuushambulia mpunga. Ndege huyu anaitwa Chiriku. Chiriku alipomwona panzi alimtamani sana, alitaka kumla. Basi alianza jitihada za kumvizia ili amkamate. Panzi aligundua nia na ujanja wa Chiriku. Bila kuchelewa alimwambia, “rafiki yangu Chiriku, tafadhali sana naomba usinile, mimi napenda kuishi”.
Chiriku aliendelea kurukaruka huku na huku kwa lengo hilo hilo la kumvizia Panzi. Bila kuchoka, Panzi naye aliendelea kumsihi sana asimle. Kwa bahati mbaya, maombi ya Panzi kwa Chiriku hayakupokelewa, yaligonga mwamba. Panzi alipoona dhamira ya Chiriku haijabadilika, alijitahidi kujaribu kumkwepa zaidi, akaruka tena, lakini Chiriku naye hakuacha kuruka huku akimlenga huyo Panzi. Hatimaye, Chiriku alibahatika kumdaka Panzi, kisha akamla.
Baada ya shibe, Chiriku aliruka na kwenda kupumzika kwenye mti. Shibe ilipopungua, Chiriku aliamua kuondoka pale mtini. Alipojaribu kuruka alishindwa, …. Du, kumbe alikuwa amenaswa kwenye ulimbo. Ilikuwa kasheshe.
Akiwa bado amenaswa, alimwona mwenye shamba akija mbio mbio kwa furaha. Chiriku alitambua kuwa arobaini yake ilikuwa imefika. Aligundua kuwa, kumbe mwenye shamba ndiye aliyekuwa ameweka mitego wa ulimbo kwa ajili ya kuwanasa waharifu wa kula mpynga shambani kwake.
Mwenye shamba alipofika alifurahi sana kumwona mateka wake kwani hapo alijua amejipatia kitoweo. Chiriku kwa woga, alimgeukia mwenye shamba, huku akitetemeka, akamwamvbia, “Naomba usinile ndugu yangu, na mimi napenda kuishi kama wewe”. Mwenye shamba hakumsikiliza akamchukua na kwenda naye nyumbani. Chiriku alilalamika njia nzima na kumwomba amwachie.
Maneno ya Chiriku hayakumgusa mwenye shamba. Alipofika nyumbani, Chiriku hakuacha kumlilia, aliendelea kuomboleza kwa sauti ya uchungu na huruma. Wakati huo huo, mawazo yalimjia Chiriku. Alikumbuka ukatili aliokuwa amemfanyia Panzi. Alikumbuka jinsi Panzi alivyokuwa akiomboleza asiliwe na vile ambavyo hakumsikiliza. Hii ina maana kuwa alitambua maana ya usemi usemao, ukimtendea mwenzio ubaya nawe jiandae, kwani utakurudia siku moja. Haya ndiyo yaliyokuwa yakitembea sasa kichwani kwa Chiriku. Alichanganyikiwa na kuogopa adhabu iliyo mbele yake.
Baadae mwenye shamba alijawa na huruma, alimfungulia na kumwacha huru. Chiriku alimshukuru sana mwenye shamba, hakuamini macho yake. Bila kuchelewa, aliruka kwa spidi kali kuelekea porini.
Kisa hiki kinatufundisha kwamba ubaya haulipi. Tunaaswa kuwa hata kama tumetendewa mabaya tusilipe kwa mabaya, bali tulipe kwa mema. Pamoja na mpunga wake kuliwa na Chiriku, bado mwenye shamba alimsamehe Chiriku, alisikiliza kilio chake cha kuomba msamaha. Maisha ndivyo yanatakiwa yawe. Makosa hutendwa na wote, bila kusameheana, itakuwa vurugu tupu.
Vilevile ukifanya jambo baya huwa halitoki moyoni na litakukosesha amani kwa muda mrefu. Tunaona kwenye kisa hiki pale Chiriku alipokumbuka ubaya aliomfanyia Panzi. Kumbe tendo ka kumla Panzi, bado lilikuwa linamuumiza moyoni mwake. Hakutaka kumsikiliza Panzi, pamoja na kuomba kote asimle.
Kutokana na kisa hiki, tunajifunza kuwa yatupasa tujitahidi kufanya yafuatayo:
1. Tuwe na utayari wa kusamehe pale tunapoombwa kufanya hivyo. Pamoja na kwamba mifano hii ni ya Chiriku na Panzi, inatugusa binadamu pia. Wengi huwa hatuko tayari kusamehe wenzetu wanapotukosea. Tujifunze kusamehe ili nasi tuweze kusamehewa.
2. Msamaha malipo yake ni faraja na amani. Kutokusamehe wenzetu kunaacha kumbukumbu na mateso yasiyofutika mioyoni mwetu. Tunaweza kujifanya tumesahau mabaya tuliyowatendea wenzetu. Utafika wakati, pamoja na kujifanya tumesahau, tutakumbuka yale mabaya yote tuliyowatendea wenzetu. Maisha yetu yatakosa amani kwani mara kwa mara tutakuwa tunakumbuka. Msamaha, utatuwezesha kuishi maisha mazuri na yenye amani, sisi na familia zetu na majirani wanaotuzunguka. Hakuna kitu muhimu kama furaha na amani. Sote yatupasa tuitafute kwa udi na uvumba.
The Healing Hands Project
The Healing Hands empowers people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community – alleviating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain free mental health services in underserved communities and promote the economic empowerment of trained grandmothers who implementing #WHO #mhGAP evidence-based psychosocial interventions. The project provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources, referrals, advocacy and awareness raising delivered through arts. Clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection