Mwongo Huwa Hasemi Yake

Simulizi
by Alfreda George (Wisdom&Wellness Counselor - TEWWY).
Mtu mwongo ni yule mtu ambaye anapenda kuongea mambo ya wenzake kwa ushabiki. Mara nyingi huwa anaongea katika mithili ya kumdhalilisha mtu. Watu wa aina hii huwa wana asili ya kuwa na marafiki wengi ambao huvutiwa na stori zake za uongo. Huo ni ubinadamu wa watu ambao hawajitambui. Mara nyingi, kinachofanyika hapo huwa ni unafiki mtupu.
Alikuwepo kaka mmoja ambaye alikuwa anaishi na dadake pamoja na dada wa kazi nyumbani kwake. Dada wa kazi alikuwa anatoka kwenye familia ya mke wake. Kaka huyo pamoja na mke wake walijaliwa na Mungu watoto wawili. Baadae huyo kaka alipata uhamisho wa muda kwenda nje ya jiji la Dar es Salaam. Aliondoka peke yake bila familia yake. Familia yake ilibaki maana walikuwa wakiishi kwenye nyumba yao walioijenga.
Wakati mume anaondoka kwenda uhamishoni, mke wake alikuwa na mimba, lakini ilikuwa bado changa. Kwa bahati mbaya, mimba hiyo iliharibika. Lakini yule dada hakumwambia wifi yake yale yaliyomsibu. Badala yake alimwambia yule dada wa kazi. Kama tunavyojua, duniani hakuna siri ya watu wawili. Yule dada wa kazi alimtonya wifi mtu. Wifi mtu alikuja juu vibaya sana. Alimwambia kuwa hapaswi kumwambia dada wa kazi mambo mazito kama hayo. Aliendelea kwa kusema kuwa, mambo hayo angepaswa kumwambia yeye, ambaye ni wifi yake, na si vinginevyo. Hakuishia hapo kwani yule wifi alimfungulia risala ndefu na kumtukana matusi ya nguoni. Kama vile matusi hayakutosha, kilichofuatia ni kupeleka taarifa za uongo kwa kaka yake. Aliongeza na chumvi kwa kusema kuwa "Mke wako ni malaya sana na kwamba, anadiriki hata kuingiza wanaume ndani ya nyumba yenu ya ndoa."
Kutokana na uzushi huo, ndoa ilianza kuyumba. Mume alianza kuwa na vituko vya ajabu kwa mke wake. Kwa kusema kweli, alikuwa haeleweki kabisa. Ni miaka mawili sasa mume haonekani nyumbani. Bahati nzuri mke alikuwa ni mtumishi wa umma, hivyo alikuwa anayamudu maisha yake. Yaani yale mabaya yote yaliyokuwa yakifanywa na dada mtu, yalikuwa yanageuzwa pale yanapofikishwa kwa kaka yake. Yalionekana ni mambo mabaya aiyokuwa akifanya wiki yake, yaani mke wa kaka yake.
Lakini, ikumbukwe kuwa Mungu hamfichi mnafiki. Ilitokea siku moja, jirani ambaye waliyekuwa wanapanga naye hayo mambo, nafsi ilimsuta. Aliona ni vema amweleze kila kitu, yaani ukweli wote. Alimweleza kuwa yale yote aliyokuwa akiambiwa na dada yake ni ya uongo mtupu. Aliendelea kwa kusema, "Umekuwa unamshutumu bure mkeo kwani yeye hafanyi hayo mambo machafu unayoelezwa, bali yeye na dada yake ndio huwa wanayafanya". Hivyo alimsihi sana huyo kijana kutoamini mambo yoyote kutoka kwa dada yake, kwani yote yalikuwa ni uzushi mtupu.
Mume aiamini maneno ya yule mama. Kwa ghadhabu, alimfukuza dada yake pamoja na yule dada wa kazi kwani na yeye alikuwa na mchango mkubwa sana katika kuifarakanisha familia hiyo ambayo haina hatia. Uongo wao umewaumbua vibaya sana. Sasa hivi wamebaki wakiona haya sana na wanashindwa kumwangalia huyo kaka na mke wake. Wamebaki hawana hata mahali pa kuweka nyuso zao. Fundisho kuu hapa ni kuwa binadamu, yatupasa tuache uongo na tusipende kuwatungia wenzetu mambo mabaya kwani ipo siku unaweza kuja kuumbuka vibaya na kusutwa hadharani. Sidhani kama kuna mtu anayependa kuumbuliwa hadharani kwani ni aibu isiyoisha milele.
The Healing Hands Project
The Healing Hands empowers people to achieve financial autonomy by building entrepreneurial skills and embedding skills transfer within the community – alleviating poverty as a driver of ill mental health. Funds raised from the jewelry will help sustain free mental health services in underserved communities and promote the economic empowerment of trained grandmothers who implementing #WHO #mhGAP evidence-based psychosocial interventions. The project provides interpersonal counseling, group talk therapy, and psychoeducation resources, referrals, advocacy and awareness raising delivered through arts. Clients learn to handcraft traditional beaded jewelry as a marketable skill. Follow us @TEWWYWisdom @WisdomWellnessCollection